Somo la Kwanza: Mwa 14:18-20
Somo la Pili: 1Kor 11:23-26
Injili Lk 9:11-17
Utangulizi:
Ndugu wapendwa leo tunaadhimisha kwa namna ya pekee sherehe ya mwili na damu ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa kufuata agizo alilotoa yeye mwenyewe; “fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (Lk 22:19). Hivyo ni karamu ya duniani na mbinguni tunapoiadhimisha kwa mastahili na kushiriki kwa ibada.
Tafakari:
Leo ndugu zangu wapendwa tunaadhimisha kwa namna ya kipekee kabisa Umungu wa Yesu katika maumbo ya Mkate na Divai. Ndio kilele cha maadhimisho yote ya kanisa. Tutazame kwa ufupi katekesi na majina ya Ekaristi Takatifu. Ekaristi Takatifu ni:
- Chemchemi na kilele cha maisha ya Kanisa: katika maadhimisho yote ya kanisa, maadhimisho ya sakramenti nyingine – zinaungana na Ekaristi na zinaelekezwa kwake. Hii ni kwa sababu katika Ekaristi Takatifu mna kila hazina ya kiroho ya kanisa, yaani Kristo mwenyewe.
- Sadaka: hii hujionyesha katika maneno yenyewe ya kuwekwa Ekaristi, “Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu, na kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu” (Lk 22:19-20). Yesu mwenyewe anasema amefanyika fidia kwa ajili yetu (Mk 10:45). Katika Ekaristi Kristo hutoa Mwili wake ule ule uliiotolewa kwa ajili yetu Msalabani, damu yake ilele iliyomwagika msalabani kwa ajili yetu.
- Tendo la Shukrani: Ekaristi ni sakramenti ya wokovu iliyotekelezwa na Kristo msalabani. Katika adhimisho la ekaristi Takatifu, kila kiumbe hutolewa kwa baba kwa njia ya Kifo na ufufuko wa Kristo. Katika fumbo hilo inatolewa sifa na shukrani katika uumbaji na katika ubinadamu.
- Kumbukumbu: tunapotolea sadaka ya misa tunaadhimisha kumbukumbu ya sadaka ya kifo chake. Tunamtolea baba kile ambacho yeye mwenyewe alitupatia. Somo laa 2, Linatueleza hayo kwamba Ekaristi takatifu ni ukumbusho wa sadaka ya Yesu Msalabani.
- Uwapo: Ekaristi takatifu ni uwepo halisi wa Yesu katika maumbo ya Mkate na divai. Katika maumbo ya mkate na Divai “mna mwili na damu ya Bwana wetu Yesu Kristo. Kweli halisi na uwamo kamili pamoja na roho na umungu, na hivi ni Kristo mzima kabisa. Hata Kama ni kipisi kidogo ni Kristo Mzima.
Hivyo tunapaswa kuiangalia Ekaristi Takatifu Kama tendo la shukrani na masifu kwa Baba, kumbukumbu ya sadaka ya Kristo na ya mwili wake, uwepo wa Kristo kwa uweza wa Neno lake na Roho wake.
Ekaristi Takatifu na majitoleo ya kikuhani. Tunapewa picha hiyo kwa Mfalme Melkisedeki katika somo la 1. Ndio maana Ekaristi Takatifu na sadaka ya upadre vinafungamana. Na pia Ekaristi Takatifu ina muunganiko na matoleo ya vipaji na majitoleo yetu.
Ekaristi inatuliza njaa na kiu ya karamu ya mbinguni. Yesu anawalisha makutano. Anatuliza njaa ambayo kwa macho ya kibinadamu na uwezo wa kibinadamu haikuwezekana. Tunaona wanafunzi wanamwaambia Yesu awaage makutano. Lakini Yesu anawalisha hataki waende bila kula. Yesu hapendi tushiriki misa takatifu bila kushiriki Ekaristi takatifu.
- Je tujiulize tunashiriki Kikamilifu Kumpokea Yesu katika Ekaristi takatifu? >Yeye alijitoa sadaka, je sisi tunajitoa – kusaidia wengine – kazini – michango mbalimbali n.k.
- Kama hatumpokei kwa nini? Ni nini kinakuzuia? je unaelewa ukuu wa Sakrament ya Ekaristi takatifu katika maisha Yako? Je ni hali yako ya ndani? vizuizi? Kwa nn wewe ukubali kurukwa tu kwa benchi kila jumapili? fanya kitu!!!!
- Paulo anatuambia – tunapopokea Ekaristi (1Kor. 10:16-17) sisi sote ingawa ni wengi tunafanywa mwili mmoja kwa kushiriki Ekaristi Takatifu- sasa ndugu zangu Mafarakano yanatoka wapi? magonvi yanatoka wapi? uzushi unatoka wapi? umbea unatoka wapi? Chuki zinatoka wapi? Zarau zinatoka wapi? ukiona hivyo… either tunampokea Yesu kwa mazoea au hatumpokei kabisa, tunaishi tu.
- Leo Tuna Maandamano Yesu anakuja nyumbani – Siku ya Kumwabudu Yesu katika maeneo yetu, tunatembea naye, tumshangilie, tumwabudu, tumshukuru kwa aliyotutendea, anayotutendea, katika familia, shughuli, mateso, mahangaiko, tumtolee maombi yetu. Ni nafasi ya pekee, wewe unayekosa siku ya kuabudu, kukaa na Yesu, leo ni Fursa: Yeye ni mwenye Huruma, ni daktari ni mwalimu, ni Mungu ni mfalme – mkabidhi maisha yako, familia, kila kitu – hakika hatakuacha amekuja kwa ajili yako.
Basi tumwombe Yesu wa Ekaristi aingie katika maisha yetu na matendo yetu, ili tufungamane naye katika kutupenda na kupendana sisi kwa sisi ambayo maana ya Ekaristi kwetu. Amina.